Skip to main content

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - FASIHI SIMULIZI

 FASIHI SIMULIZI

 


Fasihi simulizi ni moja kati ya tanzu za fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo. Katika mada hii utajifunza na kisha utaweza kubainisha tanzu na vipera vya fasihi simulizi pamoja na ufafanuzi wake. Na pia utaweza kutofautisha kati ya kipera na kipera au kati ya utanzu na utanzu.

 

Tanzu za Fasihi Simulizi

 

Fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili.

 

Tanzu za Fasihi Simulizi ni pamoja na hizi zifuatazo:

- Masimulizi/hadithi 

- Semi

- Ushairi

- Mazungumzo

- Maigizo 

- Ngomezi

 

Vipera vya Tanzu za Fasihi Simulizi

 

1. SIMULIZI/ HADITHI

 

Masimulizi ni fasihi yenye kusimulia habari fulani. Ni masimulizi ambayo yanatumia lugha ya mjazo au nathari na mtiririko wake huwa mwepesi au sahili. Urefu wa hadithi hutofautiana kutoka kitanzu/kipera kimoja hadi kingine. Kwa jumla zipo hadithi ambazo ni za kubuni na zingine za kihistoria. Baadhi ya vipera vya utanzu huu ni:

 

NGANO

 

Hizi ni hadithi za kimapokeo zitumiazo wahusika kama wanyama, miti na watu katika kuelezea au kuonya kuhusu maisha. Vijipera vya kipera hiki ni:

 

1. Istiara – hadithi ambayo maana yake ya wazi inawakilisha maana nyingine iliyofichika. Yaani hadithi nzima ni kama sitiari.

 

2. Mbazi- hadithi fupi yenye mafunzo itolewayo kama kielelezo wakati wa maongezi au wa kumkanya mtu

 

3. Kisa- hadithi fupi ya kufurahisha kuhusu tukio la kweli.

 

VISAKALE

Masimulizi ya kimapokeo juu ya wahenga au mashujaa wa kabila au taifa yenye kuchanganya chuku na historia. Kwa mfano hadithi za Liyongo

 

MAPISI

Maelezo ya historia bila kutia mambo ya kubuni.

 

SOGA

Ni hadithi ndogo ndogo zinazohusisha utani na ucheshi kwa kiasi fulani. Hizi ni hadithi ambazo hutambwa katika mtiririko wa matukio ambao huzua kicheko. Soga hudhamiria kuchekesha na pia kukejeli.

 

TARIHI

Hizi ni hadithi ambazo husimulia au zimejengwa kwenye matukio ya kihistoria. Inawezekana matukio yanayosimuliwa yakawa ya kweli, yaani yalipata kutokea kihistoria. Hadithi hizi hutokea zaidi katika maandishi.

 

VISASILI

Ni utanzu unaofungamana na imani za dini na mizungu ya jamii. Hizi ni hadithi za kale zenye kuwakilisha imani na mtazamo wa jamii inayohusika kuhusu asili ya ulimwengu na mwenendo wake, kuhusu asili yao wenyewe, na maana na shabaha ya maisha yao. Mara nyingi hadithi hizi huaminiwa kuwa ni kweli tupu, na hutumika kuelezea au kuhalalisha baadhi ya mila na madhehebu ya jamii inayohusika.

 



2. USHAIRI

 

Huu ni utanzu wa fasihi simulizi unaowasilishwa kwa hadhira kwa njia ya uimbaji au ughani badala ya usemaji wa kawaida. Katika utanzu huu kuna vipera viwili ambavyo ni nyimbo na maghani.

 

NYIMBO

 

Nyimbo ni kila kinachoimbwa. Kipera hiki kimegawanyika katika vijipera vifuatavyo ambavyo ni, tumbuizo, bembea, kongozi, nyimbo za dini, wawe, tenzi, tendi, mbolezi, kimai, nyiso, nyimbo za vita, nyimbo za uwindaji, nyimbo za taifa, nyimbo za watoto na nyimbo za kazi.

 

1. Tumbuizo: hizi ni nyimbo za furaha ziimbwazo kuwafurahisha watu kwenye matukio mbalimbali kama vile ngomani au harusini. Bembea; hizi ni nyimbo za kubembeleza watoto. Kigezo kilichotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo hulenga kubembeleza watoto.

 

2. Kongozi: hizi ni nyimbo za kuaga mwaka.

 

3. Nyimbo za dini: hizi ni nyimbo zinazoimbwa kwa lengo la kumsifu Mungu au miungu.

 

4. Wawe: hizi ni nyimbo za kilimo; huuimbwa wakati wa kulima.

 

5. Tenzi: hizi ni nyimbo ndefu za kimasimulizi au mawaidha.

 

6. Tendi: hizi ni nyimbo ndefu za masimulizi juu ya matendo ya mashujaa, wahusika wa tendi ni watu wenye historia za matendo ya kishujaa.

 

7. Mbolezi: hizi ni nyimbo za kilio au maombolezo.

 

8. Kimai: hizi ni nyimbo zihusuzo shughuli za baharini.

 

9. Nyiso: hizi ni nyimbo za jandoni.

 

10. Nyimbo za vita: hizi ni nyimbo ziimbwazo na askari wakati wa vita.

 

11. Nyimbo za watoto: hizi ni nyimbo waimbazo watoto wakati wa michezo yao.

 

12. Nyimbo za uwindaji: hizi ni nyimbo ambazo huimbwa na makundi ya wawindaji wakati wa shughuli au sherehe zao.

 

13. Nyimbo za Taifa: hizi ni nyimbo za kusifia Taifa au kabila.

 

14. Nyimbo za kazi: hizi ni nyimbo zinazoimbwa katika shughuli mbalimbali kama vile, kulima, kutwanga, kusuka, uvuvi, uashi, useremala na kadhalika

 



 

MAGHANI

 

Maghani ni istilahi inayotumiwa kuelezea aina ya ushairi ambao hutolewa kwa kalima au maneno badala ya kuimbwa. Kipera hiki kina vijipera vitatu ambavyo ni maghani ya kawaida,sifo na maghani masimulizi.

 

1. Maghani ya kawaida ni kundi ambalo tunaweza kuingiza fani mbalimbali za ushahiri simulizi kama vile ushairi wa mapenzi, siasa, maombolezo, kazi, dini ilimradi unaghanwa katika namna ya uwasilishwaji wake.

 

2. Sifo: hizi ni tungo za kusifu ambazo husifu watu, wanyama na mimea. Baadhi ya sifo huwa zinakashifu au kukejeli. Sifo huwa na tanzu muhimu kama vile vivugo (majigambo), pembe zinatondozi.

 

a) Kivugo: hili ni ghani la kujisifia, hutungwa na kughanwa na muhusika mwenyewe.

 

b) Tondozi: hizi ni tungo za kusifu watu, wanyama au vitu.

 

3. Ghani masimulizi: hizi ni ghani ambazo hutambwa ili kusimulia hadithi, historia au tukio fulani. Ghani masimulizi ina vipera vinne ambavyo ni rara, ngano, sifo na tendi.

 

a) Rara ni hadithi fupi nyepesi ya kishairi yenye visa vya kusisimua; rara huimbwa au kughanwa ikiambatana na ala za muziki.

 

b) Ngano: hizi ni hadithi za mapokeo zitumiazo wahusika kama wanyama, miti na watu katika kuelezea au kuonya kuhusu maisha.Ngano huwa ghani masimulizi inapowasilishwa pamoja na ala ya muziki.

 

c) Sifo: hizi ni tungo za kusifu: sifo huwa ghani masimulizi inapoingiza muziki katika utondozi wake, lugha iliyotumika ni lugha ya kishairi.

 

d) Tendi: hizi ni ghani ndefu za masimulizi juu ya matendo ya mashujaa yenye uzito kijamii au kitaifa.


3.
 SEMI

 

Semi ni tungo au kauli fupifupi za kisanaa zenye kubeba maana au mafunzo muhimu ya kijamii. Baadhi ya tanzu katika kundi hili ni:

 

1. Methali: Methali ni semi fupi fupi zenye kueleza kwa muhtasari fikra au mafunzo, mazito yaliyotokana na uzoefu wa kijamii. Mara nyingi mawazo hayo huelezwa kwa kutumia tamathali hasa sitiari na mafumbo. Methali nyingi huwa na muundo wenye sehemu mbili. Sehemu ya kwanza huanzisha wazo fulani, na sehemu ya pili hulikanusha au kulikaamilsha wazo hilo. Kwa mfano; mwenda pole hajikwai, aliye juu mngoje chini.

 

2. Vitendawili: Ni usemi uliofumbwa ambao hutolewa kwa hadhira ili iufumbue. Fumbo hilo kwa kawaida huwa linafahamika katika jamii hiyo, na mara nyingi lina mafunzo muhimu kwa washiriki, mbali na kuwachemsha bongo zao. Vitendawili ni sanaa inayotegemea uwezo wa mtu kutambua, kuhusisha na kulinganisha vitu vya aina mbalimbali vilivyomo katika maumbile.

 

3. Misimu: Ni semi za muda na mahali maalum ambazo huzuka na kutoweka kutegemea mazingira maalum. Msimu ukipata mashiko ya kutosha katika jamii huweza hatimaye kuingia katika kundi la methali za jamii hiyo.

 

4. Mafumbo: Ni semi za maonyo au mawaidha ambazo maana zake za ndani zimefichika. Fumbo hubuniwa na msemaji kwa shabaha na hadhira maalum, hivyo ni tofauti na methali au vitendawili ambavyo ni semi za kimapokeo.

 

4. Lakabu: Haya ni majina ya kupanga ambayo baadhi ya watu hupewa au hujipatia kutokana na sifa zao za kimwili, kinasaba, kitabia au kimatendo. Majina haya huwa ni maneno au mafungu ya maneno yenye maana iliyofumbwa. Mara nyingi majina haya huwa ni sitiari. Baadhi ya majina haya humsifia mhusika, lakini mengine humkosoa au hata kumdhalilisha; Mifano: simba wa yuda- Hali Selassie, Baba wa taifa – Mwl Nyerere.

 

4. MAIGIZO

 

Maigizo ni mchezo ambao hutumia watendaji wa kuiga tabia na matendo ya watu au viumbe wengine ili kuburudisha na kutoa ujumbe fulani kwa hadhira.

 

 

UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI SIMULIZI

 

Umuhimu wa Uhakiki wa Kazi za Fasihi Simulizi

 

Umuhimu wa uhakiki wa kazi za fasihi simulizi ni kubaini ubora wa kazi za fasihi simulizi, kubaini vipengele mbalimbali vya fani na maudhui, kupima namna kazi inavyoambatana na mazingira inamotokea, kupima kufaa na kutokufaa kwa fasihi simulizi, kubaini ukweli wa mambo yanayoelezwa, kuangalia uhalisi wa watu na mazingira katika jamii na kubaini umuhimu wa kazi ya fasihi katika jamii husika.

 

Vigezo vya Uhakiki wa Kazi za Fasihi Simulizi

 

Uhakiki wa kazi ya fasihi huzingatia vigezo viwili ambavyo vimegawanyika katika vipengele mbalimbali. Vigezo hivyo ni fani na maudhui. Katika kigezo cha fani mhakiki atazingatia muundo, mtindo, matumizi ya lugha, wahusika na mandhari wakati katika kigezo cha maudhui mhakiki atazingatia dhamira, migogoro, falsafa, msimamo na ujumbe.

 

Uhakiki wa Hadithi

 

Uhakiki wa hadithi kama ilivyo katika kazi nyingine za fasihi simulizi umejikita katika kuchunguza vipengele mbalimbali vya fani na maudhui. Vipengele vya fani ni muundo, mtindo, wahusika, mandhari na matumizi ya lugha. Aidha kwa upande wa maudhui, vipengele vyake ni dhamira, migogoro, falsafa, ujumbe na msimamo.

 

Matumizi ya Semi katika Hadithi

 

Uhakiki wa semi katika fasihi umejikita kuangalia usahihi wa matumizi ya vipengele mbalimbali vya lugha katika kazi ya fasihi inayohusika. Vipengele hivyo ni misemo, nahau na mafumbo. Vilevile uhakiki wa semi umejikita katika kuchunguza namna lugha ilivyofuzu kigezo cha kwenda na wakati.

  

 

Popular posts from this blog

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - UANDISHI WA BARUA

   UANDISHI WA BARUA     Uandishi Wa Barua   Barua za kirafiki ambazo pia huitwa za kidugu huandikwa baina ya watu wa undugu au jamii moja. Katika mada hii utaweza kujifunza muundo wa uandishi wa barua ya kirafiki na jinsi ya kuandika barua ya kirafiki. Utaweza kutofautisha kati ya barua ya kirafiki na ile isiyokuwa ya kirafiki.   BARUA ZA KIRAFIKI   Iwapo ni katika ndugu barua za kirafiki zaweza kuwa kwa watu kama: baba, mama, shangazi, mume, mke, mtoto, na kadhalika. Katika jamii waandikiwao barua za kirafiki ni kama jirani, rafiki, mpenzi, mwalimu, mwanafunzi, daktari, mgonjwa, na kadhalika.   Muundo wa Barua za Kirafiki   Mambo muhimu ya kuzingatia katika uandishi wa barua za kirafiki:   1. ANWANI kamili ya mwandishi, katika herufi hukaa juu upande wa kulia mwa karatasi.   2. TAREHE, chini ya anwani.   3. MTAJO wa heshima kwa anayeandikiwa, kama vile, mpendwa, mpenzi, na kadhalika, huandikwa kushoto, baada ya tarehe.   4. UTANGULIZI wa baru

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - USIMULIZI

  USIMULIZI Usimulizi ni jumla ya maelezo yanayotolewa na mtu au watu wengi kuhusu tukio fulani. Katika mada hii utajifunza juu ya taratibu za usimulizi wa matukio kupitia njia kuu mbili za masimulizi, yaani kwa njia ya mdomo au kwa njia ya maandishi. Pia utaweza kujifunza juu ya mbinu mbalimbali za usimulizi.   USIMULIZI WA HADITHI   Usimulizi hufanyika kwa njia kuu mbili yaani kwa njia ya maandishi na kwa njia ya masimulizi ya mdomo. Kila njia hutegemea namna msimuliaji anavyoweza kuwasiliana na msikilizaji. Ikiwa msimuliaji na msikilizaji hawakukaribiana, njia ambayo itatumika ni ile ya maandishi. Kwa mfano kama utahitaji kumweleza mtu aliyembali kuhusu tukio fulani la kusisimua utalazimika kutumia maandishi, yaani utatumia njia ya kumwandikia barua. Lakini kama unamsimulia mtu ambaye yupo karibu nawe, utatumia njia ya mazungumzo ya ana kwa ana. USIMULIZI WA HABARI   Taratibu za Usimulizi wa Matukio: Usimulizi wa matukio dhamira yake ni kumweleza mtu au watu tu

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - UFAHAMU

  UFAHAMU Ufahamu ni dhana inayorejelea kujua na kulielewa jambo kwa usahihi na kuweza kulielezea upya kwa usahihi bila kupoteza maana yake ya msingi. Ufahamu wa mtu waweza kupimwa katika kusikiliza jambo au katika kusoma.   KUSIKILIZA   Ufahamu wa kusikiliza ni zaidi ya kusikiliza tu kile kilichosemwa; badala yake ni uwezo wa mtu kuelewa maana ya maneno anayoyasikia na kuweza kuhusiana nayo kwa namna fulani. Kwa mfano mwanafunzi anaposikiliza hadithi, ufahamu mzuri wa kusikiliza humsaidia kuielewa hadithi hiyo, kuikumbuka, kuijadili, na hata kuisimulia tena kwa maneno yake mwenyewe.   Mambo ya Kuzingatia katika Ufahamu wa Kusikiliza   Ufahamu wa kusikiliza unahusisha michakato kadhaa katika kuelewa na kupata maana ya kile kinachozungumzwa. Michakato hii inahusisha:   1. Kuelewa vizuri sarufi ya lugha ile inayozungumzwa   2. Kuelewa vyema maana ya maneno ya mhusiaka anayezungumza   3. Kuelewa sintaksia (muundo wa maneno) ya sentensi kwa namna zinavyowas

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - FASIHI KWA UJUMLA

    FASIHI KWA UJUMLA   Fasihi  ni sanaa ya lugha inayoshughulikia masuala yanayomhusu binadamu matatizo yake, ndoto zake, matumaini yake, migogoro yake na jinsi anavyoingiliana na mazingira yake. (Wamitila, 2004). Fasili hii imejaribu kufafanua vizuri kile ambacho fasihi inajihusisha nacho, kimsingi fasihi inajihusisha na wanadamu. Vitu vya msingi tunavyoviona katika fasili hii ni kwamba fasihi ni sanaa, na fasihi inatumia lugha lakini zaidi fasihi inajihusisha na wanadamu. Dhima za Fasihi katika Jamii Dhima za fasihi katika jamii ni pamoja na hizi zifuatazo: 1.   Kuburudisha jamii : Pamoja na mambo mengine fasihi inalenga kuburudisha jamii. Kupitia takribani vipera vyake vyote, fasihi huwa na kusudi la kufurahisha, kutumbuiza na kusisimua hadhira, kwa mfano kupitia nyimbo, hadithi, mashairi na kadhalika. 2.   Kuelimisha .  Fasihi hutumika kama nyenzo ya kuelimisha jamii, kupitia fasihi wanajamii wanaweza kuelimishwa juu ya mambo mabalimbali, kama vile

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - AINA ZA MANENO

AINA ZA MANENO Katika lugha ya Kiswahili kuna angalau aina nane za maneno ambazo wataalamu wengi wa lugha wanakubaliana hivyo. Katika mada hii utaweza kujifunza na kubainisha aina zote nane za maneno na jinsi zinvyotumika katika sentensi. Utaweza pia kujifunza namna ya kutofautisha aina za maneno ambazo zimeleta ubishi miongoni mwa wataalamu wengi hususani katika Viunganishi na Vihusishi.   Aina Saba za Maneno ya Kiswahili                                             Aina za maneno katika lugha ya Kiswahili ni pamoja na hizi zifuatazo:   Aina Nomino (N)                                                                                                       Viwakilishi (W)    Vitenzi (T)                                                                                                                 Vivumishi (V)    Vielezi (E)  Viunganishi (U)   Vihusishi (H) Vihisishi (I)   Ufafanuzi wa Aina za Maneno   1.   NOMINO (N)   Nomino ni maneno yanayotaj

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - MAWASILIANO

MAWASILIANO Katika mada hii unatarajiwa kuelewa fasili ya mawasiliano na jinsi mchakato wa mawasiliano unavyofanyika. Utaelewa dhana ya lugha na vipengele muhimu vinavyokamilisha fasili ya lugha. Utaelewa dhima kuu za lugha, matumizi na umuhimu wake. Vilevile katika mada hii utajifunza juu ya lafudhi na matamshi mbalimbali ya watumiaji wa lugha ya Kiswahili. Lugha kama Chombo cha Mawasiliano Mawasiliano ni mchakato wa kuhawilisha taarifa kwa njia ya ubadilishanaji wa mawazo, hisia, malengo, tabia, matarajio, mitazamo kupitia mazungumzo, ishara na maandishi. Ni ubadilishanaji wa taarifa unaoleta maana baina ya pande mbili au zaidi ambazo zinaweza kuwa viumbe hai au kinyume chake. Sasa hapa sisi tutajikita katika mawasiliano yanayofanywa baina ya viumbe wanaotumia lugha (ambao kimsingi ni binadamu). Maana ya Mawasiliano Lugha ni nyenzo muhimu sana katika mawasiliano ya binadamu. Ulishawahi kujiuliza kwamba mwasiliano yangekuwaje pasipokuwepo lugha? Mwalimu angekua anatumia mt