Skip to main content

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - UANDISHI WA BARUA

   UANDISHI WA BARUA

 

 

Uandishi Wa Barua

 Barua za kirafiki ambazo pia huitwa za kidugu huandikwa baina ya watu wa undugu au jamii moja. Katika mada hii utaweza kujifunza muundo wa uandishi wa barua ya kirafiki na jinsi ya kuandika barua ya kirafiki. Utaweza kutofautisha kati ya barua ya kirafiki na ile isiyokuwa ya kirafiki.

 

BARUA ZA KIRAFIKI

 

Iwapo ni katika ndugu barua za kirafiki zaweza kuwa kwa watu kama: baba, mama, shangazi, mume, mke, mtoto, na kadhalika. Katika jamii waandikiwao barua za kirafiki ni kama jirani, rafiki, mpenzi, mwalimu, mwanafunzi, daktari, mgonjwa, na kadhalika.

 

Muundo wa Barua za Kirafiki

 

Mambo muhimu ya kuzingatia katika uandishi wa barua za kirafiki:

 

1. ANWANI kamili ya mwandishi, katika herufi hukaa juu upande wa kulia mwa karatasi.

 

2. TAREHE, chini ya anwani.

 

3. MTAJO wa heshima kwa anayeandikiwa, kama vile, mpendwa, mpenzi, na kadhalika, huandikwa kushoto, baada ya tarehe.

 

4. UTANGULIZI wa barua yenyewe ambao kwa desturi huwa ni salamu.

 

5. BARUA YENYEWE ambayo ndiyo kiini cha waraka.

 

6. SALAMU za kumalizia, pengine kwa jamaa na jamii.

 

7. HITIMISHO, katika aya, maalumu ambayo huwa, kwa mfano: ‘Ni mimi baba yako akupendaye, na kadhalika.

 

8. SAHIHI ambayo si sharti wala muhimu sana.

 

9. JINA au MAJINA ya mwandishi, mwishoni.

 



Tazama mfano wa barua ya kirafiki:

 

Mfano 1

 

MUSOMA FISH PACK

S.L.P 4546

MUSOMA

23/5/2013

 

Mwanangu Nyamchele,

Ninafuraha kukujulisha kuwa nimepokea barua yako. Mambo yote uliyoyaeleza nimeyaelewa barabara. Huku nyumbani sote tu wazima na ni matumaini yetu kwamba afya yako ni nzuri.

 

Tabia ya kulalamikia chakula ni mbaya. Tabia kama hii ikikomaa husababisha ulafi. Kumbuka hukwenda shuleni kula kama nguruwe. Huko shuleni nimekupeleka ili usome kwa bidii na ujifunze mengi. Usitamani kustarehe na kufikiria maakuli na anasa zingine za ulimwengu huu. Ondoa fikira za chakula akilini mwako na uache uzembe, eboo!

 

Hebu nikuonye kuhusu kuwapima na kuwachagua walimu. Walimu katika shule hiyo ni wabobezi na ndio maana nikakupeleka hapo. Wanajua mnayostahili kufundishwa. Huna ruhusa ya kusema eti walimu wengine ni wakali na hufundisha haraka haraka sana. Wewe unahitaji kutega sikio na kutii. Ukiwa makini na uwe na imani utayaelewa mambo unayofundishwa. Usisahau kuwa mchagua jembe si mkulima.

 

Mambo makubwa unayostahili kuyatilia bidii ni masomo yako. Muda wa miaka minne ni mfupi sana. Uonyeshe adabu njema kila wakati. Uwaonyeshe walimu wako taadhima na uwatii daima dawamu.

 

Jambo lililo kubwa katika shughuli yoyote ni uvumilivu. Ukivumilia utavuna matunda mabivu. Sitachoka kukusisitizia, ‘Ukilima pantosha, utavuna pankwisha.’ Fanya kila jitihada utimize mambo mengi iwezekanavyo kuanzia leo lakini usipapie chochote. Ndo ndo ndo hujaza ndoo.

 

Mungu akubariki. Umwombe akusaidie katika kila jambo. Ujiepushe na maovu yoyote yale. Ukiwa na jambo usiwe na hofu kutuarifu mara moja. Mama yako amekusalimu sana. Amenikumbusha nikupashe hakuna refu lisilo na ncha.

Kwaheri kwa sasa.

 

Ni mimi, baba yako akupendaye,

Magafu Malima

  

 

Popular posts from this blog

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - AINA ZA MANENO

AINA ZA MANENO Katika lugha ya Kiswahili kuna angalau aina nane za maneno ambazo wataalamu wengi wa lugha wanakubaliana hivyo. Katika mada hii utaweza kujifunza na kubainisha aina zote nane za maneno na jinsi zinvyotumika katika sentensi. Utaweza pia kujifunza namna ya kutofautisha aina za maneno ambazo zimeleta ubishi miongoni mwa wataalamu wengi hususani katika Viunganishi na Vihusishi.   Aina Saba za Maneno ya Kiswahili                                             Aina za maneno katika lugha ya Kiswahili ni pamoja na hizi zifuatazo:   Aina Nomino (N)                                                                   ...

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - UANDISHI WA INSHA

    UANDISHI WA INSHA   Uandishi Wa Insha   Uandishi ni kitendo cha kupangilia maneno katika maandishi. Mada hii inazungumzia uandishi wa insha za wasifu kwa umahususi wake. Kabla ya kuanza uandishi utajifunza mambo muhimu yanayopaswa kuzingatiwa katika uandishi wa insha kwa ujumla. Utaelewa muundo wa insha na mwisho utajifunza juu ya dhana ya insha ya wasifu na namna inavyoandikwa na mwisho kabisa utaangalia mfano wa insha ya wasifu.   Insha za Wasifu Insha ya wasifu ni ile ya kutoa maelezo juu ya jinsi mtu au kitu kilivyo, tabia, vitendo na mandhari (sura ya mahali jinsi panavyoonekana). Mambo muhimu katika insha ya wasifu ni: sura, rangi, umbo, vipimo, tabia, na kadhalika. Insha hizi zinaweza kuongelea kitu chochote kile, inaweza kuwa ni mnyama, mtu, Shule, nchi na kadhalika. Hatua za Uandishi wa Insha Kabla ya kuanza kuandika insha, ni muhimu sana uamue unataka kuandika juu ya nini. Inafaa uchague ile mada iliyo rahisi kwako kuweza kujieleza kik...

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - MAWASILIANO

MAWASILIANO Katika mada hii unatarajiwa kuelewa fasili ya mawasiliano na jinsi mchakato wa mawasiliano unavyofanyika. Utaelewa dhana ya lugha na vipengele muhimu vinavyokamilisha fasili ya lugha. Utaelewa dhima kuu za lugha, matumizi na umuhimu wake. Vilevile katika mada hii utajifunza juu ya lafudhi na matamshi mbalimbali ya watumiaji wa lugha ya Kiswahili. Lugha kama Chombo cha Mawasiliano Mawasiliano ni mchakato wa kuhawilisha taarifa kwa njia ya ubadilishanaji wa mawazo, hisia, malengo, tabia, matarajio, mitazamo kupitia mazungumzo, ishara na maandishi. Ni ubadilishanaji wa taarifa unaoleta maana baina ya pande mbili au zaidi ambazo zinaweza kuwa viumbe hai au kinyume chake. Sasa hapa sisi tutajikita katika mawasiliano yanayofanywa baina ya viumbe wanaotumia lugha (ambao kimsingi ni binadamu). Maana ya Mawasiliano Lugha ni nyenzo muhimu sana katika mawasiliano ya binadamu. Ulishawahi kujiuliza kwamba mwasiliano yangekuwaje pasipokuwepo lugha? Mwalimu angekua anatumia mt...

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - UFAHAMU

  UFAHAMU Ufahamu ni dhana inayorejelea kujua na kulielewa jambo kwa usahihi na kuweza kulielezea upya kwa usahihi bila kupoteza maana yake ya msingi. Ufahamu wa mtu waweza kupimwa katika kusikiliza jambo au katika kusoma.   KUSIKILIZA   Ufahamu wa kusikiliza ni zaidi ya kusikiliza tu kile kilichosemwa; badala yake ni uwezo wa mtu kuelewa maana ya maneno anayoyasikia na kuweza kuhusiana nayo kwa namna fulani. Kwa mfano mwanafunzi anaposikiliza hadithi, ufahamu mzuri wa kusikiliza humsaidia kuielewa hadithi hiyo, kuikumbuka, kuijadili, na hata kuisimulia tena kwa maneno yake mwenyewe.   Mambo ya Kuzingatia katika Ufahamu wa Kusikiliza   Ufahamu wa kusikiliza unahusisha michakato kadhaa katika kuelewa na kupata maana ya kile kinachozungumzwa. Michakato hii inahusisha:   1. Kuelewa vizuri sarufi ya lugha ile inayozungumzwa   2. Kuelewa vyema maana ya maneno ya mhusiaka anayezungumza   3. Kuelewa sintaksia (muundo wa m...

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - FASIHI SIMULIZI

  FASIHI SIMULIZI   Fasihi simulizi ni moja kati ya tanzu za fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo. Katika mada hii utajifunza na kisha utaweza kubainisha tanzu na vipera vya fasihi simulizi pamoja na ufafanuzi wake. Na pia utaweza kutofautisha kati ya kipera na kipera au kati ya utanzu na utanzu.   Tanzu za Fasihi Simulizi   Fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili.   Tanzu za Fasihi Simulizi ni pamoja na hizi zifuatazo: - Masimulizi/hadithi  - Semi - Ushairi - Mazungumzo - Maigizo  - Ngomezi   Vipera vya Tanzu za Fasihi Simulizi   1.  SIMULIZI/ HADITHI   Masimulizi ni fasihi yenye kusimulia habari fulani. Ni masimulizi ambayo yanatumia lugha ya mjazo au nathari na mtiririko wake huwa mwepesi au sahili. Urefu wa hadithi hutofautiana k...

KISWAHILI KIDATO CHA KWANZA - FASIHI KWA UJUMLA

    FASIHI KWA UJUMLA   Fasihi  ni sanaa ya lugha inayoshughulikia masuala yanayomhusu binadamu matatizo yake, ndoto zake, matumaini yake, migogoro yake na jinsi anavyoingiliana na mazingira yake. (Wamitila, 2004). Fasili hii imejaribu kufafanua vizuri kile ambacho fasihi inajihusisha nacho, kimsingi fasihi inajihusisha na wanadamu. Vitu vya msingi tunavyoviona katika fasili hii ni kwamba fasihi ni sanaa, na fasihi inatumia lugha lakini zaidi fasihi inajihusisha na wanadamu. Dhima za Fasihi katika Jamii Dhima za fasihi katika jamii ni pamoja na hizi zifuatazo: 1.   Kuburudisha jamii : Pamoja na mambo mengine fasihi inalenga kuburudisha jamii. Kupitia takribani vipera vyake vyote, fasihi huwa na kusudi la kufurahisha, kutumbuiza na kusisimua hadhira, kwa mfano kupitia nyimbo, hadithi, mashairi na kadhalika. 2.   Kuelimisha .  Fasihi hutumika kama nyenzo ya kuelimisha jamii, kupitia fasihi wanajamii wanaweza kuelimishwa j...